Gamboshi, Kijiji kinachobeba dhana ngumu kuaminika

on Thursday, April 14, 2016 - No comments:


Wakazi wa kijiji cha Gamboshi
Wengi tumekuwa tukisikia habari nyingi kuhusu kijiji cha Gamboshi kilichopo wilayani Bariadi.Kijiji hichi kimekuwa kikihusishwa na uchawi na ushirikina huku ikisemwa kuwa kina maajabu mengi sana.Kwa wale waliokuwa wakisikiliza  kipindi cha sitosahau kupitia Redio Free Afrika kipindi kile watakuwa wamewahi kusikia habari kuhusu maajabu ya kijiji hicho, mwandishi nguli wa hadithi nchini Eric Shigongo aliwahi kuandika hadithi akitumia jina la kijiji hicho.
Kuna wale ambao walikuwa wakihisi kuwa jina hilo ni la kubuni na hakuna kijiji kama hicho.
Nimekuwekea makala iliyowahi kuwekwa kwenye gazeti la mwananchi miaka kadhaa iliyopita . isome hapa chini;

Kijiji hicho ambacho ni nadra sana kutembelewa, kimepata umaaurufu mkubwa ndani na nje ya nchi kikielezwa kuwa ni kitovu cha uchawi na wachawi wanaoweza kufanya miujuza, hali ambayo imekifanya kijiji hicho kupitwa na mkondo wa kimaendeleo. 
“Sisi ni wakulima wakarimu wa pamba, mahindi na mpunga. Yote mnayoyasikia kwamba sisi ni magwiji wa uchawi ni uvumi uliotiwa chumvi nyingi. Tunamwomba Rais wetu kwa kushirikiana na Mbunge wetu, Andrew Chenge watusadie kulisafisha jina letu,”alisihi Zephania Maduhu, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Gamboshi. 

Maduhu pamoja na wanakijiji wenzake walidai kuwa, hofu iliyoenezwa ndani na nje ya nchi kuhusua uchawi uliovuka mipaka wa Kijiji cha Gamboshi umesababisha madhara makubwa kwa kijiji chao kiasi chakutengwa na jamii yote ya Watanzania. 
 “Hakuna aliyetembelea kijiji hiki kwa miaka mingi sana. Hata sisi tunapotoka nje ya kijiji, wengi hawataki kutusogelea wakiamini tutawadhuru, ” alisema Musa Deus (26), mmoja wa wakulima walionufaika kilimo cha mkataba kijijini Gamboshi.

Kwa mujibu wa Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho, tangu Uhuru mwaka 1961, hakuna kiongozi yoyote wakitaifa aliyewahi kukanyaga kijijini hapo. 

Anaongeza kuwa mtu wa pekee aliyewahi kuzuru kijijini hapo ni mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge, aliyefika kijijini hapo mwaka 2010, wakati akifanya kampeni za ubunge. 

“Tume ya Katiba ilitupita, mwenge wa Uhuru nao haujawahi kupita hapa. Tuko kisiwani mbali na Watanzania wengine,” anasema Maduhu. 

Kikiwa mafichoni kabisa, kiasi cha kilometa 44 kutoka mjini Bariadi, Kijiji cha Gamboshi si rafiki wa watu wa Kanda ya Ziwa kama ambavyo Mwananchi Jumapili ilibaini katika utafiti wake wa muda mrefu. 

Mijini na vijijini, kumekwepo na ubishani mkali kuhusu ni mkoa gani unaokimiliki kijiji hicho, ambacho baadhi ya wakazi wake wanadai kuwa miongoni mwa vioja vyake ni mauzauza yanayoweza kuifanya Gamboshi ionekane kama Jiji la New York, Marekani au London, Uingereza wakati wa usiku. 
Pamoja na umaarufu wake, bado uwepo wa Gamboshi umekuwa ni kitendawili kikubwa kwa jamii ya Wasukuma kutoka mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Simiyu. 

Mbali na ubishani mkali kuhusu kuhusu mahali hasa kilipo kijiji hicho cha miujiza, wengi wamekuwa wakidai wakazi wake siyo jamii ya Kisukuma. 

Wakazi wa Shinyanga wanadai kuwa Gamboshi iko wilayani Magu, Mkoa wa Mwanza, wakati wale Mwanza wakidai kuwa iko mkoani Shinyanga.

Kwa mujibu wa Maduhu, Gamboshi iko katika Wilaya Bariadi, karibu na mpaka unaotenganisha na Wilaya ya Magu iliyoko mkoani Mwanza. 

“Tunaomba sana ndugu mwandishi, waambie Watanzania kuwa mengi wanayoyasikia kuhusu Gamboshi siyo kweli kabisa. Tunawakaribisha wote waje hapa kufanya biashara na sisi, waoleane na vijana wa Gamboshi kama wafanyavyo katika vijiji vingine. Sisi ni binadamu wema,” anasema mkazi wa kijiji hicho, Malimi Kidimi ambaye ni mkulima.

Ofisa Mkaguzi kutoka Bodi ya Pamba (TCB), Ramadhani Dissa, anaielezea Gamboshi kuwa ni moja ya vijiji vilivyouza pamba nyingi msimu huu.
 
Anasema kuwa Wilaya ya Bariadi, kilipo kijiji hicho, imeweza kuuza robo ya pamba yote iliyouzwa nchi nzima hadi kufikia katikati ya Oktoba mwaka huu. 

Kwa mujibu wa Dissa ni maofisa wa bodi ya pamba tu ndiyo wanaofika kijijini hapo na kwamba siyo wananchi tu wanaogopa kufika hapo, bali hata baadhi ya kampuni za ununuzi wa pamba. 

“Kampuni ya Billlchard, moja ya mawakala wa kilimo cha mkatabaka alishindwa kutuletea mbolea hapa, badala yake akaenda kuibwaga katika Kituo cha Polisi Bariadi kwa kile ambacho wafanyakazi wake walidai ni kuhofia usalama wao,”anasema Maduhu. 

“Pigo tulilopata kutokana sifa mbaya tuliyobambikiziwa haisemeki na madhara makubwa tunayapata kutokana na kutengwa na jamii. Wanakijiji wa Gamboshi ni masikini kwa sababu mkondo wa maendeleo na mageuzi umepata mbali sana nao,” anasisitiza Maduhu. 

Chanzo cha hofu
Akifafanua kiini cha chuki na hofu hiyo, Maduhu alidai kuwa hapo zamani ilitokea kijana mmoja kutoka kijiji jirani cha Ngasamwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na msichana mzaliwa wa Gamboshi. 
“Siku moja kijana huyo alikuja kijijini hapa akimsandikiza mpenzi wake, kisha kushindwa kurudi kijijini mwake,” anasimulia Maduhu akiongeza, “Juhudi za kumsaka kijina huyo hazikiweza kuzaa matunda, hadi aliponekana kichakani baada ya siku saba, huku ngozi yake imebadilika na kuwa nyeupe.” 

Anaeleza kuwa alipouliza alifikaje kichakani hapo, kijana huyo alijibu kuwa ameteremshwa na ndege kutoka Ulaya na baada ya hapo kijana huyo alirukwa na akili na kushindwa kuuongea. 

“Ilibidi achukuliwe na kupelekwa kutibiwa na waganga wa jadi na akapona baada ya matibabu ya zaidi ya mwezi mmoja,” anasema Maduhu akieleza kuwa kisa hicho kilitiwa chumvi nyingi licha ya kuwa na ukweli kiasi. 

Anasema kuwa, tangu siku hiyo Gamboshi ikatangaziwa uadui na vijiji vingine kiasi cha kukifanya kuogopwa na kuchukiwa. 

“Uvumi kama Gamboshi inaweza kuonekana kama Ulaya au Marekani ulianzia hapo na umendelea kurudifiwa na kukikifanyakijiji hiki kiitwe jiji la maajabu,” alidai Maduhu. 

Sisi ni wasafi
Mkazi mwingine wa kijiji hicho, Malimi Kidima anasema kuwa wana Gamboshi wangeweza kuitangazia dunia kuwa wao ni wasafi lakini, kwa miaka mingi wamekosa jinsi ya kuifanya sauti yao isikike.
 
Hakuna redio wala Luninga
“Redio ndiyo njia ya pekee inayotufanya sisi tuwe karibu na dunia, Hakuna mwenye luninga hapa kwa sababu hakuna umeme. Tunasoma magezeti kupitia vichwa vya habari vinavyosomwa kila siku redioni,” anasema Kidima.

Mkazi wa Lamadi, wilayani Magu, Anthony Mashimba alidai: “Gamboshi ni jiji la ‘masupastaa’ wa uchawi hawatakuachia ufike huko.” 

Tofauti na wengine, Mkurugenzi wa Bodi ya Pamba ya Kanda ya Ziwa, Jones Bwahama alitoa uhakika na kusema Gamboshi imekuwa ikifikiwa mara kwa mara.
Mauza mauza ya kwanza
Kutoka Bariadi mjini ni lazima upitie kijiji cha Ngulyati kiasi cha kilometa 30 Mashariki ya Bariadi katika barabara itokayo Bariadi kwenda Magu.

Hakuna kibao kinachotambulisha Kijiji cha Gamboshi mwanzoni mwa barabara ya vumbi inayoelekea Gamboshi kuanzia Ngulyati. 

Watu walikuwa wengi katika kilometa 5 za awali kuelekea Gamboshi, lakini idadi ikazidi kupunguia kwa namna tulivyozidi kukikaribia kijiji hicho. 

Barabara ilikuwa tupu hadi kilometa tano kukufikia Gamboshi hali ambayo ilianzisha hofu mpya hata kwa mwandishi wa makala haya. 

Nyumba nzuri mfano wa shule za kisasa za ‘English Medium’ ilionekana kuvutia macho kilometa chache kabla ya kukifikia Kijiji cha Gamboshi. 

“Ile ni shule ya Serikali au ya mtu binafsi,” aliuliza mmoja wa watu tuliokuwa nao katika safari hiyo baada ya macho yake kuishuhudia kwa mbali.
Lakini kwa mshango dereva alisema: “Hakuna shule yoyote ule ni mlima tu wa mawe mengi.” 

Ilioneka dhahiri kuwa ni nyumba, lakini hata tulipopiga picha kwa kamera niliyokuwa nayo, picha ilionesha kuwa hakuna nyumba yeyote. 

Baada ya mwendo, Kijiji cha Gamboshi kikaanza kuonekana kikipambwa na miti ya Jakaranda yenye maua mekundu, kiliioenekana ni kijiji kizuri, chenye nyumba chache na hali yake kunogeshwa na ubaridi uliotokana na miti mirefu iliyopandwa kuzunguka nyumba chache zilizokuwepo.

Habari hii imenukuliwa kwenye tovuti ya Mwananchi kupitia gazeti lake la Mwananchi Jumapili, kama ilivyoandikwa na mwandishi Miguel Suleyman.

Tagged as: ,
Unknown About Unknown

“You have no idea how much the last few days have meant to me," I began. "Meeting you has been the best thing that's ever happened to me.” Get the latest entertainment updates from Best Hope Media or call +255 655 987 588

Get Updates

Subscribe to our e-mail newsletter to receive updates.

Share This Post

Related posts

0 comments:

Like, share and send to friends